Categories
Zaburi

Zaburi 60

Kuomba Kuokolewa

Kwa mwimbishaji. Mtindo wa “Shushani Eduthi.” Utenzi wa Daudi wa kufundisha. Wakati alipopigana na Waaramu kutoka Aramu-Naharaimu na Aramu-Soba, naye Yoabu akarudi nyuma na kuwaua Waedomu 12,000 katika Bonde la Chumvi.

1 Ee Mungu, umetukataa na kutokea ghafula juu yetu,

umekasirika: sasa turejeshe upya!

2 Umetetemesha nchi na kuipasua;

uiponye mavunjiko yake, kwa maana inatetemeka.

3 Umewaonyesha watu wako nyakati za kukata tamaa;

umetunywesha mvinyo unaotuyumbisha.

4 Kwa wale wanaokucha wewe,

umewainulia bendera,

ili iweze kutwekwa dhidi ya upinde.

5 Tuokoe na utusaidie kwa mkono wako wa kuume,

ili wale uwapendao wapate kuokolewa.

6 Mungu amenena kutoka patakatifu pake:

“Nitaigawa Shekemu kwa ushindi

na kulipima Bonde la Sukothi.

7 Gileadi ni yangu na Manase ni yangu;

Efraimu ni kofia yangu ya chuma,

nayo Yuda ni fimbo yangu ya utawala.

8 Moabu ni sinia langu la kunawia,

juu ya Edomu natupa kiatu changu;

nashangilia kwa kushindwa kwa Ufilisti.”

9 Ni nani atakayenipeleka hadi mji wenye ngome?

Ni nani atakayeniongoza hadi nifike Edomu?

10 Ee Mungu, si ni wewe uliyetukataa sisi,

na hutoki tena na majeshi yetu?

11 Tuletee msaada dhidi ya adui,

kwa maana msaada wa mwanadamu haufai kitu.

12 Kwa msaada wa Mungu tutapata ushindi,

naye atawaponda adui zetu.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/60-1f5cd29a55f6c20cc05ab78c548a317c.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 61

Kuomba Ulinzi

Kwa mwimbishaji. Kwa ala za nyuzi za uimbaji. Zaburi ya Daudi.

1 Ee Mungu, sikia kilio changu,

usikilize maombi yangu.

2 Kutoka miisho ya dunia ninakuita,

ninaita huku moyo wangu unadhoofika;

uniongoze kwenye mwamba

ule ulio juu kuliko mimi.

3 Kwa kuwa umekuwa kimbilio langu,

ngome imara dhidi ya adui.

4 Natamani kukaa hemani mwako milele,

na kukimbilia chini ya uvuli wa mbawa zako.

5 Ee Mungu, kwa kuwa umesikia nadhiri zangu,

umenipa urithi wa wale wanaoliogopa jina lako.

6 Mwongezee mfalme siku za maisha yake,

miaka yake kwa vizazi vingi.

7 Yeye na atawazwe kwenye kiti cha enzi mbele za Mungu milele;

amuru upendo wako na uaminifu wako vimlinde.

8 Ndipo daima nitaliimbia sifa jina lako

na kuzitimiza nadhiri zangu siku baada ya siku.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/61-3ac274c7c3493b29ad55324abf7cd5cb.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 62

Mungu Kimbilio La Pekee

Kwa mwimbishaji. Mtindo wa Yeduthuni. Zaburi ya Daudi.

1 Kwa Mungu peke yake nafsi yangu inapata pumziko;

wokovu wangu watoka kwake.

2 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu;

yeye ni ngome yangu, sitatikisika kamwe.

3 Mtamshambulia mtu hata lini?

Je, ninyi nyote mtamtupa chini,

ukuta huu ulioinama na uzio huu unaotikisika?

4 Walikusudia kikamilifu kumwangusha

toka mahali pake pa fahari;

wanafurahia uongo.

Kwa vinywa vyao hubariki,

lakini ndani ya mioyo yao hulaani.

5 Ee nafsi yangu, upumzike, kwa Mungu peke yake,

tumaini langu latoka kwake.

6 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu;

ndiye ngome yangu, sitatikisika.

7 Wokovu wangu na heshima yangu viko kwa Mungu,

ndiye mwamba wangu wenye nguvu

na kimbilio langu.

8 Enyi watu, mtumainini yeye wakati wote,

miminieni mioyo yenu kwake,

kwa kuwa Mungu ni kimbilio letu.

9 Binadamu wa ngazi ya chini ni pumzi tu,

nao wa ngazi ya juu ni uongo tu;

wakipimwa kwenye mizani, si chochote;

wote kwa pamoja ni pumzi tu.

10 Usitumainie vya udhalimu

wala usijivune kwa vitu vya wizi;

ingawa utajiri wako utaongezeka,

usiviwekee moyo wako.

11 Jambo moja Mungu amelisema,

mambo mawili nimeyasikia:

kwamba, Ee Mungu,

wewe una nguvu,

12 na kwamba, EeBwana,

wewe ni mwenye upendo.

Hakika utampa kila mtu thawabu

kwa kadiri ya alivyotenda.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/62-a950032ccaebbb5077ac681c630c0766.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 63

Shauku Kwa Ajili Ya Uwepo Wa Mungu

Zaburi ya Daudi. Wakati alipokuwa katika Jangwa la Yuda.

1 Ee Mungu, wewe ni Mungu wangu,

nakutafuta kwa moyo wote;

nafsi yangu inakuonea kiu,

mwili wangu unakuonea wewe shauku,

katika nchi kame na iliyochoka

mahali ambapo hapana maji.

2 Nimekuona katika mahali patakatifu

na kuuona uwezo wako na utukufu wako.

3 Kwa sababu upendo wako ni bora kuliko uhai,

midomo yangu itakuadhimisha.

4 Nitakusifu siku zote za maisha yangu,

na kwa jina lako nitainua mikono yangu.

5 Nafsi yangu itatoshelezwa

kama kwa wingi wa vyakula;

kwa midomo iimbayo

kinywa changu kitakusifu wewe.

6 Kitandani mwangu ninakukumbuka wewe,

ninawaza juu yako makesha yote ya usiku.

7 Kwa sababu wewe ndiwe msaada wangu,

chini ya uvuli wa mbawa zako naimba.

8 Nafsi yangu inaambatana nawe,

mkono wako wa kuume hunishika.

9 Wale wanaotafuta uhai wangu wataharibiwa,

watakwenda chini kwenye vilindi vya dunia.

10 Watatolewa wafe kwa upanga,

nao watakuwa chakula cha mbweha.

11 Bali mfalme atafurahi katika Mungu,

wale wote waapao kwa jina la Mungu watamsifu,

bali vinywa vya waongo vitanyamazishwa.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/63-bb48ec067525b38ebabf85dc1e30c3ea.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 64

Kuomba Ulinzi Dhidi Ya Maadui

Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.

1 Ee Mungu, unisikie ninapoeleza lalamiko langu,

uyahifadhi maisha yangu kutokana na vitisho vya adui.

2 Unifiche kutokana na shauri la siri la waovu,

kutokana na zile kelele za kundi la watenda mabaya.

3 Wananoa ndimi zao kama panga

na kuelekeza maneno yao kama mishale ya kufisha.

4 Hurusha mishale kutoka kwenye mavizio kwa mtu asiye na hatia,

humrushia ghafula bila woga.

5 Kila mmoja humtia moyo mwenzake

katika mipango mibaya;

huzungumza juu ya kuficha mitego yao,

nao husema, “Ni nani ataiona?”

6 Hufanya shauri baya la dhuluma na kusema,

“Tumebuni mpango mkamilifu!”

Hakika nia na moyo wa mwanadamu vina hila.

7 Bali Mungu atawapiga kwa mishale,

nao ghafula wataangushwa.

8 Atageuza ndimi zao wenyewe dhidi yao

na kuwaleta kwenye maangamizi;

wote wawaonao watatikisa vichwa vyao

kwa dharau.

9 Wanadamu wote wataogopa,

watatangaza kazi za Mungu

na kutafakari yale aliyoyatenda.

10 Wenye haki na wafurahi katikaBwana,

na wakimbilie kwake;

wanyofu wote wa moyo na wamsifu yeye!

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/64-0954e5e1243e91350d7b817e5d554bc1.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 65

Kusifu Na Kushukuru

Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. Wimbo.

1 Ee Mungu, sifa zakungojea katika Sayuni;

kwako wewe nadhiri zetu zitatimizwa.

2 Ewe usikiaye maombi,

kwako wewe watu wote watakuja.

3 Tulipokuwa tumefunikwa kabisa na dhambi,

wewe ulisamehe makosa yetu.

4 Heri wale uliowachagua

na kuwaleta karibu ili waishi katika nyua zako!

Tunashibishwa kwa mema ya nyumba yako,

mema ya Hekalu lako takatifu.

5 Unatujibu kwa matendo ya kushangaza ya haki,

Ee Mungu Mwokozi wetu,

tumaini la miisho yote ya duniani

na la bahari zilizo mbali sana,

6 uliyeumba milima kwa uwezo wako,

ukiwa umejivika nguvu,

7 uliyenyamazisha dhoruba za bahari,

ngurumo za mawimbi yake,

na ghasia za mataifa.

8 Wale wanaoishi mbali sana

wanaogopa maajabu yako,

kule asubuhi ipambazukiapo

na kule jioni inakofifilia

umeziita nyimbo za furaha.

9 Waitunza nchi na kuinyeshea,

waitajirisha kwa wingi.

Vijito vya Mungu vimejaa maji

ili kuwapa watu nafaka,

kwa maana wewe umeviamuru.

10 Umeilowesha mifereji yake

na kusawazisha kingo zake;

umeilainisha kwa manyunyu

na kuibariki mimea yake.

11 Umeuvika mwaka taji ya baraka,

magari yako yanafurika kwa wingi.

12 Mbuga za majani za jangwani umezineemesha;

vilima vimevikwa furaha.

13 Penye nyanda za malisho pamejaa makundi ya wanyama,

na mabonde yamepambwa kwa mavuno;

vyote vinashangilia kwa furaha na kuimba.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/65-f12412d24536665e5d22b9fcfae35ba2.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 66

Kusifu Mungu Kwa Ajili Ya Wema Wake

Kwa mwimbishaji. Wimbo. Zaburi.

1 Mpigieni Mungu kelele za shangwe, dunia yote!

2 Imbeni utukufu wa jina lake;

mpeni sifa zake kwa utukufu!

3 Mwambieni Mungu, “Jinsi gani yalivyo ya kutisha matendo yako!

Uwezo wako ni mkuu mno kiasi kwamba

adui wananyenyekea mbele zako.

4 Dunia yote yakusujudia,

wanakuimbia wewe sifa,

wanaliimbia sifa jina lako.”

5 Njooni mwone yale Mungu aliyoyatenda,

mambo ya kutisha aliyoyatenda

miongoni mwa wanadamu!

6 Alifanya bahari kuwa nchi kavu,

wakapita kati ya maji kwa miguu,

njooni, tumshangilie.

7 Yeye hutawala kwa uwezo wake milele,

macho yake huangalia mataifa yote:

waasi wasithubutu kujiinua dhidi yake.

8 Enyi mataifa, msifuni Mungu wetu,

sauti ya sifa yake isikike,

9 ameyahifadhi maisha yetu

na kuizuia miguu yetu kuteleza.

10 Ee Mungu, wewe ulitujaribu,

ukatusafisha kama fedha.

11 Umetuingiza kwenye nyavu

na umetubebesha mizigo mizito

migongoni mwetu.

12 Uliwaruhusu watu watukalie vichwani,

tulipita kwenye moto na kwenye maji,

lakini ulituleta kwenye nchi

iliyojaa utajiri tele.

13 Nitakuja hekaluni mwako na sadaka za kuteketezwa

na kukutimizia nadhiri zangu:

14 nadhiri ambazo midomo yangu iliahidi

na nilizotamka kwa kinywa changu

nilipokuwa katika shida.

15 Nitakutolea dhabihu za wanyama wanono

na sadaka za kondoo dume,

nitakutolea mafahali na mbuzi.

16 Njooni msikilize ninyi nyote mnaomcha Mungu,

nami niwaambie aliyonitendea.

17 Nilimlilia kwa kinywa changu,

sifa zake zilikuwa katika ulimi wangu.

18 Kama ningekuwa nimeyaficha maovu moyoni mwangu,

Bwana asingekuwa amenisikiliza;

19 lakini hakika Mungu amenisikiliza

na amesikia sauti yangu katika maombi.

20 Sifa apewe Mungu,

ambaye hakulikataa ombi langu

wala kunizuilia upendo wake!

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/66-70ae261997c556379da49c61557244d9.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 67

Mataifa Yahimizwa Kumsifu Mungu

Kwa mwimbishaji. Na ala za nyuzi za muziki. Zaburi. Wimbo.

1 Mungu aturehemu na kutubariki,

na kutuangazia nuru za uso wake,

2 ili njia zako zijulikane duniani,

wokovu wako katikati ya mataifa yote.

3 Ee Mungu, mataifa na wakusifu,

mataifa yote na wakusifu.

4 Mataifa yote wafurahi na kuimba kwa shangwe,

kwa kuwa unatawala watu kwa haki

na kuongoza mataifa ya dunia.

5 Ee Mungu, mataifa na wakusifu,

mataifa yote na wakusifu.

6 Ndipo nchi itatoa mazao yake,

naye Mungu, Mungu wetu, atatubariki.

7 Mungu atatubariki

na miisho yote ya dunia itamcha yeye.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/67-2c582af6264c83c4cba031743f9b97c6.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 68

Wimbo Wa Taifa Wa Shangwe Kwa Ushindi

Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. Wimbo.

1 Mungu na ainuke, watesi wake watawanyike,

adui zake na wakimbie mbele zake.

2 Kama vile moshi upeperushwavyo na upepo,

vivyo hivyo uwapeperushe mbali,

kama vile nta iyeyukavyo kwenye moto,

vivyo hivyo waovu na waangamie mbele za Mungu.

3 Bali wenye haki na wafurahi,

washangilie mbele za Mungu,

wafurahi na kushangilia.

4 Mwimbieni Mungu, liimbieni sifa jina lake,

mtukuzeni yeye aendeshwaye juu ya mawingu:

jina lake niBwana,

furahini mbele zake.

5 Baba wa yatima, mtetezi wa wajane,

ni Mungu katika makao yake matakatifu.

6 Mungu huwaweka wapweke katika jamaa,

huwaongoza wafungwa wakiimba,

bali waasi huishi katika nchi kame.

7 Ee Mungu, ulipowatangulia watu wako,

ulipopita nyikani,

8 dunia ilitikisika,

mbingu zikanyesha mvua,

mbele za Mungu, Yule wa Sinai,

mbele za Mungu, Mungu wa Israeli.

9 Ee Mungu, ulinyesha mvua nyingi

na kuiburudisha ardhi iliyokuwa imechoka.

10 Ee Mungu, watu wako waliishi huko,

nawe kwa wingi wa utajiri wako

uliwapa maskini mahitaji yao.

11 Bwana alitangaza neno,

waliolitangaza neno hilo walikuwa kundi kubwa:

12 “Wafalme na majeshi walikimbia upesi,

watu waliobaki kambini waligawana nyara.

13 Hata ulalapo katikati ya mioto ya kambini,

mabawa ya njiwa wangu yamefunikwa kwa fedha,

manyoya yake kwa dhahabu ingʼaayo.”

14 Wakati Mwenyezialipowatawanya wafalme katika nchi,

ilikuwa kama theluji iliyoanguka juu ya Salmoni.

15 Milima ya Bashani ni milima iliyotukuka,

milima ya Bashani ina vilele vilivyochongoka.

16 Enyi milima yenye vilele vilivyochongoka,

kwa nini mnakazia macho kwa wivu,

katika mlima Mungu anaochagua kutawala,

ambakoBwanamwenyewe ataishi milele?

17 Magari ya Mungu ni makumi ya maelfu,

na maelfu ya maelfu;

Bwana amekuja kutoka Sinai

hadi katika patakatifu pake.

18 Ulipopanda juu, uliteka mateka,

ukapokea vipawa kutoka kwa wanadamu,

hata kutoka kwa wale walioasi,

ili wewe, EeBwanaMungu, upate kuishi huko.

19 Sifa apewe Bwana, Mungu Mwokozi wetu,

ambaye siku kwa siku hutuchukulia mizigo yetu.

20 Mungu wetu ni Mungu aokoaye,

BwanaMwenyezi hutuokoa na kifo.

21 Hakika Mungu ataponda vichwa vya adui zake,

vichwa vya hao waendao katika njia za dhambi.

22 Bwana alisema, “Nitawarudisha kutoka Bashani;

nitawarudisha kutoka vilindi vya bahari,

23 ili uweze kuchovya miguu yako katika damu ya adui zako,

huku ndimi za mbwa wako zikiwa na fungu lake.”

24 Ee Mungu, maandamano yako yameonekana,

maandamano ya Mungu wangu, Mfalme wangu,

yakielekea patakatifu pake.

25 Mbele wako waimbaji, baada yao wapiga vinanda,

pamoja nao wako wanawali wakipiga matari.

26 Msifuni Mungu katika kusanyiko kubwa,

msifuniBwanakatika kusanyiko la Israeli.

27 Liko kabila dogo la Benyamini likiwaongoza,

wakifuatwa na kundi kubwa la watawala wa Yuda,

hatimaye watawala wa Zabuloni na Naftali.

28 Ee Mungu, amuru uwezo wako,

Ee Mungu tuonyeshe nguvu zako,

kama ulivyofanya hapo awali.

29 Kwa sababu ya Hekalu lako Yerusalemu

wafalme watakuletea zawadi.

30 Mkemee mnyama aliyeko kwenye manyasi,

kundi la mafahali katikati ya ndama za mataifa.

Na walete minara ya madini ya fedha wakinyenyekea.

Tawanya mataifa yapendayo vita.

31 Wajumbe watakuja kutoka Misri,

Kushiatajisalimisha kwa Mungu.

32 Mwimbieni Mungu, enyi falme za dunia,

mwimbieni Bwana sifa,

33 mwimbieni sifa yeye apandaye mbingu za kale zilizo juu,

yeye angurumaye kwa sauti kuu.

34 Tangazeni uwezo wa Mungu,

ambaye fahari yake iko juu ya Israeli,

ambaye uwezo wake uko katika anga.

35 Ee Mungu, wewe unatisha katika mahali patakatifu pako,

Mungu wa Israeli huwapa watu wake uwezo na nguvu.

Mungu Asifiwe!

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/68-d8dfb1c4c99c05a6b89a1af668daac70.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 69

Kilio Cha Kuomba Msaada Wakati Wa Dhiki

Kwa mwimbishaji. Mtindo wa “Yungiyungi.” Zaburi ya Daudi.

1 Ee Mungu, niokoe,

kwa maana maji yamenifika shingoni.

2 Ninazama kwenye vilindi vya matope,

pasipo mahali pa kukanyaga,

Nimefika kwenye maji makuu,

mafuriko yamenigharikisha.

3 Nimechoka kwa kuomba msaada,

koo langu limekauka.

Macho yangu yanafifia,

nikimtafuta Mungu wangu.

4 Wale wanaonichukia bila sababu

ni wengi kuliko nywele za kichwa changu;

wengi ni adui kwangu bila sababu,

wale wanaotafuta kuniangamiza.

Ninalazimishwa kurudisha

kitu ambacho sikuiba.

5 Ee Mungu, wewe unajua upumbavu wangu,

wala hatia yangu haikufichika kwako.

6 Ee Bwana, eweBwanaMwenye Nguvu Zote,

wakutumainio wasiaibishwe

kwa ajili yangu;

wakutafutao wasifedheheshwe kwa ajili yangu,

Ee Mungu wa Israeli.

7 Kwa maana nimestahimili dharau kwa ajili yako,

aibu imefunika uso wangu.

8 Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu,

mgeni kwa wana wa mama yangu mwenyewe.

9 Kwa kuwa wivu wa nyumba yako unanila,

matukano ya wale wanaokutukana yameniangukia.

10 Ninapolia na kufunga,

lazima nivumilie matusi.

11 Ninapovaa nguo ya gunia,

watu hunidharau.

12 Wale wanaoketi mlangoni wananisimanga,

nimekuwa wimbo wa walevi.

13 Lakini EeBwana, ninakuomba,

kwa wakati ukupendezao;

katika upendo wako mkuu, Ee Mungu,

unijibu kwa wokovu wako wa hakika.

14 Uniokoe katika matope,

usiniache nizame;

niokoe na hao wanichukiao,

kutoka kwenye vilindi vya maji.

15 Usiache mafuriko yanigharikishe

au vilindi vinimeze,

au shimo lifumbe kinywa chake juu yangu.

16 EeBwana, unijibu, kwa wema wa upendo wako;

kwa huruma zako nyingi unigeukie.

17 Usimfiche mtumishi wako uso wako,

uharakishe kunijibu, kwa sababu niko katika shida.

18 Njoo karibu uniokoe,

nikomboe kwa sababu ya adui zangu.

19 Unajua jinsi ninavyodharauliwa,

kufedheheshwa na kuaibishwa,

adui zangu wote unawajua.

20 Dharau zimenivunja moyo

na nimekata tamaa,

nimetafuta wa kunihurumia, lakini sikumpata,

wa kunituliza, lakini sikumpata.

21 Waliweka nyongo katika chakula changu

na walinipa siki nilipokuwa na kiu.

22 Meza iliyoandaliwa mbele yao na iwe mtego,

nayo iwe upatilizo na tanzi.

23 Macho yao yatiwe giza ili wasiweze kuona,

nayo migongo yao iinamishwe daima.

24 Uwamwagie ghadhabu yako,

hasira yako kali na iwapate.

25 Mahali pao na pawe ukiwa,

wala asiwepo yeyote atakayeishi katika mahema yao.

26 Kwa kuwa wanawatesa wale uliowajeruhi,

na kuzungumza juu ya maumivu ya wale uliowaumiza.

27 Walipize uovu juu ya uovu,

usiwaache washiriki katika wokovu wako.

28 Wafutwe kutoka kitabu cha uzima

na wasiorodheshwe pamoja na wenye haki.

29 Mimi niko katika maumivu na dhiki;

Ee Mungu, wokovu wako na unihifadhi.

30 Nitalisifu jina la Mungu kwa wimbo,

nami nitamtukuza kwa kumtolea shukrani.

31 Hili litampendezaBwanakuliko ngʼombe dume,

zaidi ya fahali akiwa na pembe na kwato zake.

32 Maskini wataona na kufurahi:

ninyi mnaomtafuta Mungu, mioyo yenu na iishi!

33 Bwanahuwasikia wahitaji

wala hadharau watu wake waliotekwa.

34 Mbingu na dunia zimsifu,

bahari na vyote viendavyo ndani yake,

35 kwa maana Mungu ataiokoa Sayuni

na kuijenga tena miji ya Yuda.

Kisha watu watafanya makao yao humo na kuimiliki,

36 watoto wa watumishi wake watairithi

na wale wote walipendao jina lake

wataishi humo.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/69-14c7d602a9ec7a028a4fa2d12acf7a7d.mp3?version_id=1627—