Categories
Zaburi

Zaburi 50

Ibada Ya Kweli

Zaburi ya Asafu.

1 Mwenye Nguvu, Mungu,Bwana,

asema na kuiita dunia,

tangu mawio ya jua

hadi mahali pake liendapo kutua.

2 Kutoka Sayuni, penye uzuri mkamilifu,

Mungu anaangaza.

3 Mungu wetu anakuja na hatakaa kimya,

moto uteketezao unamtangulia,

akiwa amezungukwa na tufani kali.

4 Anaziita mbingu zilizo juu,

na nchi, ili aweze kuwahukumu watu wake:

5 “Nikusanyieni watu wangu waliowekwa wakfu,

waliofanya agano nami kwa dhabihu.”

6 Nazo mbingu zinatangaza haki yake,

kwa maana Mungu mwenyewe ni hakimu.

7 “Sikieni, enyi watu wangu, nami nitasema,

ee Israeli, nami nitashuhudia dhidi yenu:

Mimi ndimi Mungu, Mungu wenu.

8 Sikukemei kwa sababu ya dhabihu zako,

au sadaka zako za kuteketezwa,

ambazo daima ziko mbele zangu.

9 Sina haja ya fahali wa banda lako,

au mbuzi wa zizi lako.

10 Kwa maana kila mnyama wa msituni ni wangu,

na pia makundi ya mifugo juu ya vilima elfu.

11 Ninamjua kila ndege mlimani,

nao viumbe wa kondeni ni wangu.

12 Kama ningekuwa na njaa, nisingewaambia ninyi,

kwa maana ulimwengu ni wangu,

pamoja na vyote vilivyomo ndani yake.

13 Je, mimi hula nyama ya mafahali

au kunywa damu ya mbuzi?

14 Toa sadaka za shukrani kwa Mungu,

timiza nadhiri zako kwake Yeye Aliye Juu Sana,

15 na uniite siku ya taabu;

nami nitakuokoa, nawe utanitukuza.”

16 Lakini kwake mtu mwovu, Mungu asema:

“Una haki gani kunena sheria zangu

au kuchukua agano langu midomoni mwako?

17 Unachukia mafundisho yangu

na kuyatupa maneno yangu nyuma yako.

18 Unapomwona mwizi, unaungana naye,

unapiga kura yako pamoja na wazinzi.

19 Unakitumia kinywa chako kwa mabaya

na kuuongoza ulimi wako kwa hila.

20 Wanena daima dhidi ya ndugu yako

na kumsingizia mwana wa mama yako.

21 Mambo haya unayafanya, nami nimekaa kimya,

ukafikiri Mimi nami ni kama wewe.

Lakini nitakukemea

na kuweka mashtaka mbele yako.

22 “Yatafakarini haya, ninyi mnaomsahau Mungu,

ama sivyo nitawararua vipande vipande,

wala hapatakuwepo na yeyote wa kuwaokoa:

23 Atoaye dhabihu za shukrani ananiheshimu mimi,

naye aiandaa njia yake

ili nimwonyeshe wokovu wa Mungu.”

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/50-ce8e48aa383d466ec190c7d8544492a7.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 51

Kuomba Msamaha

Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. Baada ya kukemewa na nabii Nathani kwa kuzini na Bathsheba.

1 Ee Mungu, unihurumie,

kwa kadiri ya upendo wako usiokoma,

kwa kadiri ya huruma yako kuu,

uyafute makosa yangu.

2 Unioshe na uovu wangu wote

na unitakase dhambi yangu.

3 Kwa maana ninajua makosa yangu,

na dhambi yangu iko mbele yangu daima.

4 Dhidi yako, wewe peke yako, nimetenda dhambi

na kufanya yaliyo mabaya machoni pako,

ili uthibitike kuwa wa kweli unenapo,

na kuwa na haki utoapo hukumu.

5 Hakika mimi nilizaliwa mwenye dhambi,

mwenye dhambi tangu nilipotungwa mimba kwa mama yangu.

6 Hakika wewe wapendezwa na kweli itokayo moyoni,

ndani sana ya moyo wangu wanifundisha hekima.

7 Nioshe kwa hisopo, nami nitakuwa safi,

unisafishe, nami nitakuwa mweupe kuliko theluji.

8 Unipe kusikia furaha na shangwe,

mifupa uliyoiponda na ifurahi.

9 Ufiche uso wako usizitazame dhambi zangu,

na uufute uovu wangu wote.

10 Ee Mungu, uniumbie moyo safi,

uifanye upya roho ya uthabiti ndani yangu.

11 Usinitupe kutoka mbele zako

wala kuniondolea Roho wako Mtakatifu.

12 Unirudishie tena furaha ya wokovu wako,

unipe roho ya utii, ili initegemeze.

13 Ndipo nitakapowafundisha wakosaji njia zako,

na wenye dhambi watakugeukia wewe.

14 Ee Mungu, Mungu uniokoaye,

niokoe na hatia ya kumwaga damu,

nao ulimi wangu utaimba juu ya haki yako.

15 EeBwana, fungua midomo yangu,

na kinywa changu kitatangaza sifa zako.

16 Wewe hupendezwi na dhabihu, au ningaliileta,

hufurahii sadaka za kuteketezwa.

17 Bali dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika,

moyo uliovunjika wenye toba,

Ee Mungu, hutaudharau.

18 Kwa wema wa radhi yako uifanye Sayuni istawi,

ukazijenge upya kuta za Yerusalemu.

19 Hapo ndipo kutakapokuwa na dhabihu za haki,

sadaka nzima za kuteketezwa za kukupendeza sana,

pia mafahali watatolewa

madhabahuni mwako.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/51-d7e86911e361376b39ce500423ad55e4.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 52

Hukumu Ya Mungu

Kwa mwimbishaji. Utenzi wa Daudi. Baada ya Doegi, Mwedomu kumwendea Sauli na kumjulisha kuwa: “Daudi amekwenda nyumbani kwa Ahimeleki.”

1 Ewe jitu, mbona unajivunia ubaya?

Kwa nini unajivuna mchana kutwa,

wewe ambaye ni fedheha mbele za Mungu?

2 Ulimi wako hupanga mashauri mabaya ya maangamizi.

Ni kama wembe mkali, ninyi mfanyao hila.

3 Unapenda mabaya kuliko mema,

uongo kuliko kusema kweli.

4 Unapenda kila neno lenye kudhuru,

ewe ulimi wenye hila!

5 Hakika Mungu atakushusha chini

kwa maangamizi ya milele:

atakunyakua na kukuondoa kwa nguvu

kutoka hema yako,

atakungʼoa kutoka nchi ya walio hai.

6 Wenye haki wataona na kuogopa,

watamcheka, wakisema,

7 “Huyu ni yule mtu ambaye

hakumfanya Mungu kuwa ngome yake,

bali alitumainia wingi wa utajiri wake,

na akawa hodari kwa kuwaangamiza wengine!”

Neema Ya Mungu

8 Lakini mimi ni kama mti wa mzeituni

unaostawi katika nyumba ya Mungu,

nautegemea upendo wa Mungu usiokoma

milele na milele.

9 Nitakusifu milele kwa yale uliyoyatenda,

nitatumaini jina lako, kwa kuwa jina lako ni jema.

Nitakusifu mbele ya watakatifu wako.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/52-866b48522de5e9ba80791781fd94b645.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 53

Uovu Wa Wanadamu

Kwa mwimbishaji. Mtindo wa mahalathi. Utenzi wa Daudi.

1 Mpumbavu anasema moyoni mwake,

“Hakuna Mungu.”

Wameharibika, na njia zao ni za uovu kabisa,

hakuna hata mmoja atendaye mema.

2 Mungu anawachungulia wanadamu chini

kutoka mbinguni

aone kama wako wenye akili,

wowote wanaomtafuta Mungu.

3 Kila mmoja amegeukia mbali,

wameharibika wote pamoja,

hakuna atendaye mema.

Naam, hakuna hata mmoja!

4 Je, watendao mabaya kamwe hawatajifunza:

wale ambao huwala watu wangu

kama watu walavyo mkate,

hao ambao hawamwiti Mungu?

5 Hapo waliingiwa na hofu kuu,

ambapo hapakuwa cha kutetemesha.

Mungu alitawanya mifupa ya wale waliokushambulia;

uliwaaibisha, kwa sababu Mungu aliwadharau.

6 Laiti wokovu wa Israeli ungalikuja kutoka Sayuni!

Wakati Mungu arejeshapo wafungwa wa watu wake,

Yakobo na ashangilie, Israeli na afurahi!

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/53-b53885ea57ed4462561650e8e252af99.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 54

Kuomba Ulinzi Wa Mungu Kutokana Na Adui

Kwa mwimbishaji. Na ala za nyuzi za uimbaji. Utenzi wa Daudi. Wakati Wazifu walimwendea Sauli na kumjulisha, “Je, Daudi hajifichi miongoni mwetu?”

1 Ee Mungu uniokoe kwa jina lako,

unifanyie hukumu kwa uwezo wako.

2 Ee Mungu, sikia maombi yangu,

usikilize maneno ya kinywa changu.

3 Wageni wananishambulia,

watu wakatili wanayatafuta maisha yangu,

watu wasiomjali Mungu.

4 Hakika Mungu ni msaada wangu,

Bwana ndiye anayenitegemeza.

5 Mabaya na yawarudie wale wanaonisingizia,

kwa uaminifu wako uwaangamize.

6 Nitakutolea dhabihu za hiari;

EeBwana, nitalisifu jina lako

kwa kuwa ni vyema.

7 Kwa maana ameniokoa katika shida zangu zote,

na macho yangu yamewatazama adui zangu kwa ushindi.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/54-d49c4c9ba5831ca660230c77e7a26ee4.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 55

Maombi Ya Mtu Aliyesalitiwa Na Rafiki

Kwa mwimbishaji. Na ala za uimbaji. Utenzi wa Daudi.

1 Ee Mungu, sikiliza maombi yangu,

wala usidharau hoja yangu.

2 Nisikie na unijibu.

Mawazo yangu yananisumbua na nimehangaishwa

3 kwa sauti ya adui,

kwa kukaziwa macho na waovu,

kwa sababu wananiletea mateso juu yangu

na kunitukana kwa hasira zao.

4 Moyo wangu umejaa uchungu,

hofu ya kifo imenishambulia.

5 Woga na kutetemeka vimenizunguka,

hofu kuu imenigharikisha.

6 Nilisema, “Laiti ningekuwa na mbawa za njiwa!

Ningeruka niende mbali kupumzika.

7 Ningalitorokea mbali sana

na kukaa jangwani,

8 ningaliharakisha kwenda mahali pa salama,

mbali na tufani kali na dhoruba.”

9 EeBwana, uwatahayarishe waovu

na uwachanganyishie semi zao,

maana nimeona jeuri na ugomvi mjini.

10 Usiku na mchana wanazunguka juu ya kuta zake,

uovu na dhuluma vimo ndani yake.

11 Nguvu za uharibifu zinatenda kazi mjini,

vitisho na uongo haviondoki mitaani mwake.

12 Kama aliyenitukana ni adui yangu, ningevumilia,

kama mtu mwovu angejiinua dhidi yangu,

ningejificha asinione.

13 Kumbe ni wewe, mwenzangu,

mshiriki na rafiki yangu wa karibu,

14 ambaye awali tulifurahia ushirika mzuri,

tulipokuwa tukienda na umati hekaluni mwa Mungu.

15 Kifo na kiwajie adui zangu ghafula,

na washuke kuzimu wangali hai,

kwa maana uovu upo ndani yao.

16 Lakini ninamwita Mungu,

nayeBwanahuniokoa.

17 Jioni, asubuhi na adhuhuri

ninalia kwa huzuni,

naye husikia sauti yangu.

18 Huniokoa nikawa salama katika vita

vilivyopangwa dhidi yangu,

ingawa watu wengi hunipinga.

19 Mungu anayemiliki milele,

atawasikia na kuwaadhibu,

watu ambao hawabadilishi njia zao,

wala hawana hofu ya Mungu.

20 Mwenzangu hushambulia rafiki zake,

naye huvunja agano lake.

21 Mazungumzo yake ni laini kama siagi,

hata hivyo vita vimo moyoni mwake.

Maneno yake ni mororo kuliko mafuta,

hata hivyo ni upanga mkali uliofutwa.

22 MtwikeBwanafadhaa zako,

naye atakutegemeza,

hatamwacha kamwe mwenye haki wake aanguke.

23 Lakini wewe, Ee Mungu,

utawashusha waovu katika shimo la uharibifu.

Wenye kiu ya kumwaga damu na wenye hila,

hawataishi nusu ya siku zao.

Lakini mimi ninakutumaini wewe.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/55-3175e503e9a8a5521761076cc2711731.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 56

Kumtumaini Mungu

Kwa mwimbishaji. Mtindo wa “Njiwa mkimya wa mbali.” Utenzi wa Daudi. Baada ya kukamatwa na Wafilisti huko Gathi.

1 Ee Mungu unihurumie, maana watu wananifuatia vikali;

mchana kutwa wanazidisha mashambulizi yao.

2 Wasingiziaji wangu wananifuatia mchana kutwa,

wengi wananishambulia kwa kiburi chao.

3 Wakati ninapoogopa,

nitakutumaini wewe.

4 Katika Mungu, ambaye neno lake ninalisifu,

katika Mungu ninatumaini; sitaogopa.

Mwanadamu apatikanaye na kufa,

atanitenda nini?

5 Mchana kutwa wanayageuza maneno yangu,

siku zote wanapanga shauri la kunidhuru.

6 Wananifanyia hila, wanajificha,

wanatazama hatua zangu,

wakiwa na shauku ya kuutoa uhai wangu.

7 Wasiepuke kwa vyovyote,

Ee Mungu, katika hasira yako yaangushe mataifa.

8 Andika maombolezo yangu,

orodhesha machozi yangu katika gombo lako:

je, haya hayapo katika kumbukumbu zako?

9 Ndipo adui zangu watarudi nyuma

ninapoita msaada.

Kwa hili nitajua kwamba Mungu

yuko upande wangu.

10 Katika Mungu, ambaye neno lake ninalisifu,

katikaBwana, ambaye neno lake ninalisifu,

11 katika Mungu ninatumaini, sitaogopa.

Mwanadamu anaweza kunitenda nini?

12 Ee Mungu, nina nadhiri kwako,

nitakutolea wewe sadaka zangu za shukrani.

13 Kwa kuwa umeniokoa toka kwenye mauti

na miguu yangu kwenye kujikwaa,

ili niweze kuenenda mbele za Mungu

katika nuru ya uzima.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/56-f0003c24e12c7c001b28418bb94b4285.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 57

Kuomba Msaada

Kwa mwimbishaji. Mtindo wa “Usiharibu!” Utenzi wa Daudi. Baada ya kumponyoka Sauli pangoni.

1 Unihurumie, Ee Mungu, unihurumie,

kwa maana nafsi yangu inakukimbilia.

Chini ya uvuli wa mbawa zako nitakimbilia

mpaka maafa yapite.

2 Namlilia Mungu Aliye Juu Sana,

Mungu atimizaye makusudi yake kwangu.

3 Hutumana kutoka mbinguni na kuniokoa,

akiwakemea wale wanaonifuatilia vikali;

Mungu huutuma upendo wake na uaminifu wake.

4 Niko katikati ya simba,

nimelala katikati ya wanyama wenye njaa kuu:

watu ambao meno yao ni mikuki na mishale,

ambao ndimi zao ni panga kali.

5 Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu,

utukufu wako na uenee duniani kote.

6 Waliitegea miguu yangu nyavu,

nikainamishwa chini na dhiki.

Wamechimba shimo katika njia yangu,

lakini wametumbukia humo wao wenyewe.

7 Ee Mungu, moyo wangu ni thabiti;

nitaimba na kusifu kwa moyo wangu wote.

8 Amka, nafsi yangu!

Amka, kinubi na zeze!

Nitayaamsha mapambazuko.

9 Nitakusifu wewe, EeBwana, katikati ya mataifa;

nitaimba habari zako, katikati ya jamaa za watu.

10 Kwa maana upendo wako ni mkuu, waenea hadi mbinguni,

uaminifu wako unazifikia anga.

11 Ee Mungu, utukuzwe juu mbinguni,

utukufu wako na uwe duniani pote.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/57-1a616b85bc55b04c8c07c200ab7055be.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 58

Mungu Kuwaadhibu Waovu

Kwa mwimbishaji. Mtindo wa “Usiharibu!” Utenzi wa Daudi.

1 Enyi watawala, je, kweli mwanena kwa haki?

Je, mnahukumu kwa unyofu miongoni mwa watu?

2 La, mioyoni mwenu mnatunga udhalimu,

na mikono yenu hupima jeuri duniani.

3 Waovu ni wapotovu tangu kuzaliwa kwao,

toka tumboni mwa mama zao

ni wakaidi na husema uongo.

4 Sumu yao ni kama sumu ya nyoka,

kama ile ya fira ambaye ameziba masikio yake,

5 ambaye hatasikia sauti ya kutumbuiza ya mwaguzi,

hata kama mganga angecheza kwa ustadi kiasi gani.

6 Ee Mungu, yavunje meno katika vinywa vyao;

EeBwana, vunja meno makali ya hao simba!

7 Na watoweke kama maji yapitayo kwa kasi,

wavutapo pinde zao, mishale yao na iwe butu.

8 Kama konokono ayeyukavyo akitembea,

kama mtoto aliyezaliwa akiwa mfu,

wasilione jua.

9 Kabla vyungu vyenu havijapata moto wa kuni za miiba,

zikiwa mbichi au kavu,

waovu watakuwa

wamefagiliwa mbali.

10 Wenye haki watafurahi waonapo wakilipizwa kisasi,

watakapochovya nyayo zao katika damu ya waovu.

11 Ndipo wanadamu watasema,

“Hakika utulivu wa wenye haki bado una thawabu,

hakika kuna Mungu ahukumuye dunia.”

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/58-08ae4a791ab7ffb065875e6c58cfcf43.mp3?version_id=1627—

Categories
Zaburi

Zaburi 59

Kuomba Ulinzi Wa Mungu

Kwa mwimbishaji. Mtindo wa “Usiharibu!” Utenzi wa Daudi. Wakati Sauli alipotuma wapelelezi nyumbani mwa Daudi ili wamuue.

1 Ee Mungu, uniokoe na adui zangu,

unilinde kutokana na hao wanaoinuka dhidi yangu.

2 Uniponye na watu watendao mabaya,

uniokoe kutokana na wamwagao damu.

3 Tazama wanavyonivizia!

Watu wakali wananifanyia hila,

ingawa EeBwana, mimi sijakosea

wala kutenda dhambi.

4 Sijatenda kosa; hata hivyo wako tayari kunishambulia.

Inuka unisaidie, uone hali yangu mbaya!

5 EeBwanaMwenye Nguvu Zote, Mungu wa Israeli!

Zinduka uyaadhibu mataifa yote,

usionyeshe huruma kwa wasaliti.

6 Hurudi wakati wa jioni,

wakibweka kama mbwa,

wakiuzurura mji.

7 Tazama yale wanayotema kutoka vinywa vyao,

hutema upanga kutoka midomo yao,

nao husema, “Ni nani atakayetusikia?”

8 Lakini wewe,Bwana, uwacheke;

unayadharau mataifa hayo yote.

9 Ee nguvu yangu, ninakutazama wewe,

wewe, Ee Mungu, ndiwe ngome yangu,

10 Mungu wangu unipendaye.

Mungu atanitangulia,

naye atanifanya niwachekelee

wale wanaonisingizia.

11 Lakini usiwaue, EeBwana, ngao yetu,

au sivyo watu wangu watasahau.

Katika uwezo wako wafanye watangetange

na uwashushe chini.

12 Kwa ajili ya dhambi za vinywa vyao,

kwa ajili ya maneno ya midomo yao,

waache wanaswe katika kiburi chao.

Kwa ajili ya laana na uongo wanaotamka,

13 wateketeze katika ghadhabu,

wateketeze hadi wasiwepo tena.

Ndipo itakapofahamika katika miisho ya dunia

kwamba Mungu anatawala juu ya Yakobo.

14 Hurudi jioni,

wakibweka kama mbwa,

wakiuzurura mji.

15 Wanatangatanga wakitafuta chakula,

wasipotosheka hubweka kama mbwa.

16 Lakini mimi nitaziimba nguvu zako,

asubuhi nitaimba juu ya upendo wako;

kwa maana wewe ndiwe ngome yangu

na kimbilio langu wakati wa shida.

17 Ee uliye Nguvu zangu, ninakuimbia sifa.

Wewe, Ee Mungu, ndiwe ngome yangu,

Mungu unipendaye.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PSA/59-00e3ed39a1437da771044d392663d592.mp3?version_id=1627—