Categories
Mithali

Mithali 30

Misemo Ya Aguri

1 Misemo ya Aguri mwana wa Yake, usia:

Huyu mtu alimwambia Ithieli,

naam, kwa Ithieli na kwa Ukali:

2 “Mimi ni mjinga kuliko wanadamu wote;

sina ufahamu wa kibinadamu.

3 Sijajifunza hekima,

wala sina maarifa ya kumjua yeye Aliye Mtakatifu.

4 Ni nani ameshapanda mbinguni na kushuka?

Ni nani ameshakusanya upepo

kwenye vitanga vya mikono yake?

Ni nani ameshafungia maji kwenye nguo yake?

Ni nani ameimarisha miisho yote ya dunia?

Jina lake ni nani, na mwanawe anaitwa nani?

Niambie kama unajua!

5 “Kila neno la Mungu ni kamilifu;

yeye ni ngao kwa wale wanaomkimbilia.

6 Usiongeze kwenye maneno yake,

ama atakukemea na kukuthibitisha kuwa mwongo.

7 “Ninakuomba vitu viwili, EeBwana;

usininyime kabla sijafa:

8 Uutenge mbali nami udanganyifu na uongo;

usinipe umaskini wala utajiri,

bali unipe chakula cha kunitosha kila siku.

9 Nisije nikawa na vingi vya kuzidi nikakukana

na kusema, ‘Bwanani nani?’

Au nisije nikawa maskini nikaiba,

nami nikaliaibisha jina la Mungu wangu.

10 “Usimchongee mtumishi kwa bwana wake,

asije akakulaani, ukapatilizwa kwalo.

11 “Wako watu wale ambao huwalaani baba zao

na wala hawawabariki mama zao;

12 wale ambao ni safi machoni pao wenyewe

kumbe hawakuoshwa uchafu wao;

13 wale ambao daima macho yao ni ya kiburi,

ambao kutazama kwao ni kwa dharau;

14 wale ambao meno yao ni panga

na ambao mataya yao yamewekwa visu

kuwaangamiza maskini katika nchi,

na wahitaji kutoka miongoni mwa wanadamu.

15 “Mruba anao binti wawili waliao,

‘Nipe! Nipe!’

“Kuna vitu vitatu visivyotosheka kamwe,

naam, viko vinne visivyosema, ‘Yatosha!’:

16 Ni kaburi, tumbo lisilozaa,

nchi isiyoshiba maji kamwe,

na moto, usiosema kamwe, ‘Yatosha!’

17 “Jicho lile limdhihakilo baba,

lile linalodharau kumtii mama,

litangʼolewa na kunguru wa bondeni,

litaliwa na tai.

18 “Kuna vitu vitatu vinavyonishangaza sana,

naam, vinne nisivyovielewa:

19 Ni mwendo wa tai katika anga,

mwendo wa nyoka juu ya mwamba,

mwendo wa meli katika maji makuu ya bahari,

nao mwendo wa mtu pamoja na msichana.

20 “Huu ndio mwendo wa mwanamke mzinzi,

hula akapangusa kinywa chake na kusema,

‘Sikufanya chochote kibaya.’

21 “Kwa mambo matatu nchi hutetemeka,

naam, kwa mambo manne haiwezi kuvumilia:

22 Mtumwa awapo mfalme,

mpumbavu ashibapo chakula,

23 mwanamke asiyependwa aolewapo,

naye mtumishi wa kike achukuapo nafasi ya bibi yake.

24 “Vitu vinne duniani vilivyo vidogo,

lakini vina akili nyingi sana:

25 Mchwa ni viumbe wenye nguvu ndogo,

hata hivyo hujiwekea akiba ya chakula chao wakati wa kiangazi.

26 Pelele ni viumbe vyenye uwezo mdogo

hata hivyo hujitengenezea nyumba zao kwenye miamba.

27 Nzige hawana mfalme,

hata hivyo huenda pamoja vikosi vikosi.

28 Mjusi anaweza kushikwa kwa mkono,

hata hivyo huonekana katika majumba ya kifalme.

29 “Viko vitu vitatu ambavyo vinapendeza katika mwendo wao,

naam, vinne ambavyo hutembea kwa mwendo wa madaha:

30 simba, mwenye nguvu miongoni mwa wanyama,

asiyerudi nyuma kwa chochote;

31 jogoo atembeaye kwa maringo, pia beberu,

naye mfalme pamoja na jeshi lake lililomzunguka.

32 “Ikiwa umefanya upumbavu na ukajitukuza mwenyewe,

au kama umepanga mabaya,

basi funika mdomo wako na mkono wako.

33 Kwa maana kama vile kusukasuka maziwa hutoa siagi,

na pia kule kufinya pua hutoa damu,

kadhalika kuchochea hasira hutokeza ugomvi.”

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PRO/30-15e152ecb99384ffbe2c5150455bf405.mp3?version_id=1627—

Categories
Mithali

Mithali 31

Misemo Ya Mfalme Lemueli

1 Misemo ya Mfalme Lemueli, usia wa mama yake aliyomfundisha:

2 “Ee mwanangu, ee mwana wa tumbo langu,

ee mwana wa nadhiri zangu,

3 Usitumie nguvu zako kwa wanawake,

uhodari wako kwa wale wanaowaharibu wafalme.

4 “Ee Lemueli, haifai wafalme,

haifai wafalme kunywa mvinyo,

haifai watawala kutamani sana kileo,

5 wasije wakanywa na kusahau vile sheria inavyoamuru

na kuwanyima haki zao wote walioonewa.

6 Wape kileo wale wanaoangamia,

mvinyo wale walio na uchungu,

7 Wanywe na kusahau umaskini wao

na wasikumbuke taabu yao tena.

8 “Sema kwa ajili ya wale wasioweza kujisemea,

kwa ajili ya haki za wote walioachwa ukiwa.

9 Sema na uamue kwa haki,

tetea haki za maskini na wahitaji.”

Maneno Ya Mwisho: Mke Mwenye Sifa Nzuri

10 Mke mwenye sifa nzuri, ni nani awezaye kumpata?

Yeye ni wa thamani sana kuliko marijani.

11 Mume wake anamwamini kikamilifu

wala hakosi kitu chochote cha thamani.

12 Humtendea mumewe mema, wala si mabaya,

siku zote za maisha yake.

13 Huchagua sufu na kitani

naye hufanya kazi kwa mikono yenye bidii.

14 Yeye ni kama meli za biashara

akileta chakula chake kutoka mbali.

15 Yeye huamka kungali bado giza

huwapa jamaa yake chakula

na mafungu kwa watumishi wake wa kike.

16 Huangalia shamba na kulinunua,

kutokana na mapato yake hupanda shamba la mizabibu.

17 Hufanya kazi zake kwa nguvu,

mikono yake ina nguvu kwa ajili ya kazi zake.

18 Huona kwamba biashara yake ina faida,

wala taa yake haizimiki usiku.

19 Huweka mikono yake kwenye pia,

navyo vidole vyake hushikilia kijiti chenye uzi.

20 Huwanyooshea maskini mikono yake

na kuwakunjulia wahitaji vitanga vyake.

21 Theluji ishukapo, hana hofu kwa ajili ya watu wa nyumbani mwake,

kwa maana wote wamevikwa nguo za kutia joto.

22 Hutengeneza mazulia ya urembo ya kufunika kitanda chake,

yeye huvaa kitani safi na urujuani.

23 Mume wake anaheshimiwa kwenye lango la mji,

aketipo miongoni mwa wazee wa nchi.

24 Hutengeneza mavazi ya kitani na kuyauza,

naye huwauzia wafanyabiashara mishipi.

25 Amevikwa nguvu na heshima,

anaweza kucheka bila kuwa na hofu kwa siku zijazo.

26 Huzungumza kwa hekima

na mafundisho ya kuaminika yapo ulimini mwake.

27 Huangalia mambo ya nyumbani mwake

wala hali chakula cha uvivu.

28 Watoto wake huamka na kumwita aliyebarikiwa,

mumewe pia humsifu, akisema:

29 “Wanawake wengi hufanya vitu vyenye sifa nzuri,

lakini wewe umewapita wote.”

30 Kujipamba ili kuvutia ni udanganyifu na uzuri unapita upesi,

bali mwanamke anayemchaBwanaatasifiwa.

31 Mpe thawabu anayostahili,

nazo kazi zake na zimletee sifa kwenye lango la mji.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/PRO/31-ecf3346235bffee3325871f0fdf858ff.mp3?version_id=1627—