Categories
Mhubiri

Mhubiri 10

1 Kama vile nzi waliokufa huacha harufu mbaya kwenye manukato,

ndivyo upumbavu kidogo huzidi nguvu hekima na heshima.

2 Moyo wa mwenye hekima huelekea kuume,

lakini moyo wa mpumbavu huelekea kushoto.

3 Hata anapotembea barabarani,

mpumbavu hukosa ufahamu

na kudhihirisha kwa kila mmoja

jinsi alivyo mpumbavu.

4 Kama hasira ya mtawala ikiwaka dhidi yako,

usiache mahali pako,

utulivu huweza kuzuia makosa mengi.

5 Kuna ubaya niliouona chini ya jua,

aina ya kosa litokalo kwa mtawala:

6 Wapumbavu kuwekwa kwenye nafasi nyingi za juu,

wakati matajiri hushika nafasi za chini.

7 Mimi nimeona watumwa wamepanda farasi,

wakati wakuu wakitembea

kwa miguu kama watumwa.

8 Yeye achimbaye shimo

aweza kutumbukia ndani yake,

yeyote abomoaye ukuta

anaweza kuumwa na nyoka.

9 Yeyote apasuaye mawe

inawezekana yakamuumiza,

yeyote apasuaye magogo

inawezekana yakamuumiza.

10 Kama shoka ni butu

na halikunolewa,

nguvu nyingi zinahitajika,

lakini ustadi utaleta mafanikio.

11 Kama nyoka akiuma kabla ya kufanyiwa uaguzi,

mwaguzi hatahitajika tena.

12 Maneno yatokayo kinywani mwa mtu mwenye hekima

yana neema,

bali mpumbavu huangamizwa

na midomo yake mwenyewe.

13 Mwanzoni maneno yake ni upumbavu,

mwishoni ni wazimu mbaya,

14 naye mpumbavu huzidisha maneno.

Hakuna yeyote ajuaye linalokuja,

ni nani awezaye kueleza ni jambo gani

litakalotokea baada yake?

15 Kazi ya mpumbavu humchosha mwenyewe,

hajui njia iendayo mjini.

16 Ole wako, ee nchi ambayo mfalme wako alikuwa mtumwa

na ambayo wakuu wako hufanya karamu asubuhi.

17 Heri wewe, ee nchi ambayo mfalme wako ni wa uzao wenye kuheshimika

na ambayo wakuu wako hula chakula kwa wakati unaofaa:

ili kupata nguvu na si kwa ajili ya ulevi.

18 Kama mtu ni mvivu paa la nyumba huinama,

kutokana na mikono milegevu, nyumba huvuja.

19 Karamu hufanywa kwa ajili ya kicheko,

nao mvinyo hufurahisha maisha,

lakini fedha ni jawabu la mambo yote.

20 Usimshutumu mfalme hata ikiwa ni katika mawazo yako,

au kumlaani tajiri katika chumba chako cha kulala,

kwa sababu ndege wa angani wanaweza kuchukua maneno yako,

naye ndege anayeruka anaweza kutoa taarifa ya yale uliyosema.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/ECC/10-5fbbca5ca6a26cbbf73b2867d8138052.mp3?version_id=1627—

Categories
Mhubiri

Mhubiri 11

Mkate Juu Ya Maji

1 Tupa mkate wako juu ya maji,

kwa maana baada ya siku nyingi

utaupata tena.

2 Wape sehemu watu saba, naam hata wanane,

kwa maana hujui ni baa gani

litakalokuwa juu ya nchi.

3 Kama mawingu yamejaa maji,

hunyesha mvua juu ya nchi.

Kama mti ukianguka kuelekea kusini

au kuelekea kaskazini,

mahali ulipoangukia,

hapo ndipo utakapolala.

4 Yeyote atazamaye upepo hatapanda,

yeyote aangaliaye mawingu hatavuna.

5 Kama vile usivyofahamu njia ya upepo,

au jinsi mwili uumbwavyo

ndani ya tumbo la mama,

vivyo hivyo huwezi kufahamu kazi ya Mungu,

Muumba wa vitu vyote.

6 Panda mbegu yako asubuhi,

nako jioni usiruhusu mikono yako ilegee,

kwa maana hujui ni ipi itakayofanikiwa,

kwamba ni hii au ni ile,

au kwamba zote zitafanikiwa sawasawa.

Mkumbuke Muumba Wako Ukiwa Bado Kijana

7 Nuru ni tamu,

tena inafurahisha macho kuona jua.

8 Hata kama mtu ataishi miaka mingi kiasi gani,

na aifurahie yote.

Lakini na akumbuke siku za giza,

kwa maana zitakuwa nyingi.

Kila kitu kitakachokuja ni ubatili.

9 Furahi ewe kijana, wakati ungali kijana,

moyo wako na ukupe furaha

katika siku za ujana wako.

Fuata njia za moyo wako

na chochote macho yako yaonayo,

lakini ujue kwamba kwa ajili ya haya yote

Mungu atakuleta hukumuni.

10 Kwa hiyo basi, ondoa wasiwasi moyoni mwako

na utupilie mbali masumbufu ya mwili wako,

kwa kuwa ujana na nguvu ni ubatili.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/ECC/11-08c8b8fb2bf4ebf3529b7a786c3319fb.mp3?version_id=1627—

Categories
Mhubiri

Mhubiri 12

1 Mkumbuke Muumba wako

siku za ujana wako,

kabla hazijaja siku za taabu,

wala haijakaribia miaka utakaposema,

“Mimi sifurahii hiyo”:

2 kabla jua na nuru,

nao mwezi na nyota havijatiwa giza,

kabla ya kurudi mawingu baada ya mvua;

3 siku ile walinzi wa nyumba watakapotetemeka,

nao watu wenye nguvu watakapojiinamisha,

wakati wasagao watakapokoma kwa sababu ya uchache,

nao wachunguliao madirishani kutiwa giza;

4 wakati milango ya kuingia barabarani itakapofungwa

na sauti ya kusaga kufifia;

wakati watu wataamshwa kwa sauti ya ndege,

lakini nyimbo zao zote zikififia;

5 wakati watu watakapoogopa kilichoinuka juu

na hatari zitakazokuwepo barabarani;

wakati mlozi utakapochanua maua

na panzi kujikokota

nawe usiwe na shauku ya kitu chochote.

Ndipo mwanadamu aiendea nyumba yake ya milele

nao waombolezaji wakizunguka barabarani.

6 Mkumbuke Muumba wako: kabla haijakatika kamba ya fedha,

au bakuli la dhahabu halijavunjika;

kabla mtungi kuvunjika kwenye chemchemi,

au gurudumu kuvunjika kisimani,

7 nayo mavumbi kurudi ardhini yalikotoka,

na roho kurudi kwa Mungu aliyeitoa.

8 Mhubiri asema, “Ubatili! Ubatili!

Kila kitu ni ubatili!”

Hitimisho La Mambo

9 Mhubiri hakuwa tu na hekima, bali aliwagawia watu maarifa pia. Alitafakari na kutafiti na akaweka katika utaratibu mithali nyingi.

10 Mhubiri alitafiti ili kupata maneno sahihi na kila alichoandika kilikuwa sawa na kweli.

11 Maneno ya wenye hekima ni kama mchokoro, mithali zao zilizokusanywa pamoja ni kama misumari iliyogongomewa ikawa imara, yaliyotolewa na Mchungaji mmoja.

12 Tena zaidi ya hayo, mwanangu, kubali maonyo, hakuna mwisho wa kutunga vitabu vingi, nako kusoma sana huuchosha mwili.

13 Hii ndiyo jumla ya maneno;

yote yamekwisha sikiwa:

Mche Mungu, nawe uzishike amri zake,

maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.

14 Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi,

pamoja na kila neno la siri,

likiwa jema au baya.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/ECC/12-994a2f19195380145c3a7bd900bc563b.mp3?version_id=1627—