Categories
Wimbo

Wimbo 3

1 Usiku kucha kwenye kitanda changu

nilimtafuta yule moyo wangu umpendaye;

nilimtafuta, lakini sikumpata.

2 Sasa nitaondoka na kuzunguka mjini,

katika barabara zake na viwanja;

nitamtafuta yule moyo wangu umpendaye.

Kwa hiyo nilimtafuta lakini sikumpata.

3 Walinzi walinikuta

walipokuwa wakizunguka mji.

Nikawauliza, “Je, mmemwona

yule moyo wangu umpendaye?”

4 Kitambo kidogo tu baada ya kuwapita

nilimpata yule moyo wangu umpendaye.

Nilimshika na sikumwachia aende

mpaka nilipomleta katika nyumba ya mama yangu,

katika chumba cha yule aliyenichukua mimba.

5 Binti za Yerusalemu, ninawaagiza

kwa paa na kwa ayala wa shambani:

Msichochee wala kuamsha mapenzi

hata yatakapotaka yenyewe.

Shairi La Tatu

6 Ni nani huyu anayekuja kutoka jangwani

kama nguzo ya moshi,

anayenukia manemane na uvumba

iliyotengenezwa kwa vikolezo vyote

vya mfanyabiashara?

7 Tazama! Ni gari la Solomoni

lisindikizwalo na mashujaa sitini,

walio wakuu sana wa Israeli,

8 wote wamevaa panga,

wote wazoefu katika vita,

kila mmoja na upanga wake pajani,

wamejiandaa kwa ajili ya hofu za usiku.

9 Mfalme Solomoni alijitengenezea gari;

alilitengeneza kwa mbao kutoka Lebanoni.

10 Nguzo zake alizitengeneza kwa fedha,

kitako chake kwa dhahabu.

Kiti chake kilipambwa kwa zambarau,

gari lake likanakshiwa njumu kwa upendo

na binti za Yerusalemu.

11 Tokeni nje, ninyi binti za Sayuni,

mkamtazame Mfalme Solomoni akiwa amevaa taji,

taji ambalo mama yake alimvika

siku ya arusi yake,

siku ambayo moyo wake ulishangilia.

—https://api-cdn.youversionapi.com/audio-bible-youversionapi/337/32k/SNG/3-92b9f3c5a11759d9568a6fa395eeeddb.mp3?version_id=1627—

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *